
INAWEZEKANA ilikuwa utani? Au ‘waliamka’ nazo?! Kweli binadamu anaweza kuvunjika mbavu (kicheko) juu ya kaburi la mpendwa wake? Mh!

ENEO LA TUKIO
Tukio hilo lililonaswa zimazima na kamera za Risasi Jumatano, lilijiri Januari Mosi, mwaka huu kwenye kaburi la Ngwea lililopo katika Makaburi ya Kihonda mjini Morogoro.
ILIVYOKUWA
Aunt ndiye aliyeanza kutia timu kwenye makaburi hayo na kukaa. Baadhi ya ‘kruu’ ya Wema, akiwemo Petit Man nayo ilifika na kuungana na Aunt.Baada ya dakika tatu, Mama la Mama, Wema aliwasili akiwa ndani ya nguo isiyokuwa ya mtoko, akakaa upande wa pili wa kaburi. Yeye na Aunt walikaa kwa kupeana ubavu.
CHA AJABU SASA
Awali ilidaiwa kuwa, kruu hiyo ilipanga kuwa baada ya kufika kwenye kaburi hilo wangefanya dua fupi kwa ajili ya kumwombea marehemu apumzike kwa amani huko aliko.Lakini cha ajabu, kabla ya ibada hiyo, Wema, Aunt na wafuasi wao walikuwa wakipiga stori za hapa na pale na katika hali ya kushangaza zaidi, ilifika mahali wakaanza kucheka kile kicheko cha kuvunjika mbavu bila shuhuda wa tukio hili kujua nini hasa kilichokuwa kikiwachekesha!

WEMA ATUMIA SIMU KUFICHA USO
Ni dhahiri kuwa, Wema alijishtukia kuwa kitendo cha kucheka juu ya kaburi hakikuwa na ujazo wa kiungwana hivyo haraka sana aliweka simu sehemu ya midomoni na kumfanya asionekane kwenye kamera kwamba alikuwa akicheka. Miwani ya jua aliyovaa pia ilimsaidia.
Wakati Wema akionesha ubinadamu huo, ‘mwenzangu na mimi’, Aunt yeye alijimalizia kiu yake ya kicheko mpaka pale alipoamua mwenyewe kuacha na si kwa kuogopa kamera wala malaika waliolizunguka kaburi lile (kama wapo) la mmoja wa marapa bora kabisa kuwahi kutokea Tanzania.
WEMA AJIELEZA KWA RISASI
Baada ya wote kuacha kucheka na kila mmoja kuchukua nafasi ya ubinadamu, paparazi wetu alimuuliza Wema ni kwa nini walionesha kuwa na furaha juu ya kaburi la staa huyo.Wema: “Tumepita hapa ili kumuombea ndugu na rafiki yetu Mangweha hivyo hatuna lengo lingine zaidi ya hilo.“Ishu ya kupiga stori na kucheka, tusingeweza kuacha kuongea eti kisa tupo kaburini, maana kila kitu lazima kijadiliwe hata kukaa hapa tumekaa kwa sababu tunafarijika kuona kaburi la mwenzetu.”
KWA NINI WALIFANYA ZIARA KABURINI KWA NGWEA?
Awali, mastaa hao na wapambe wao walikuwa na shoo ya kuukaribisha Mwaka Mpya iliyofanyika Desemba 31, 2014 ndani ya Ukumbi wa Matei Lounge mjini Dodoma.Wakiwa wanarudi Dar, walipiga kituo mjini Morogoro ambapo miongoni mwa mambo waliyokuwa nayo kwenye ratiba ni kulitembelea kaburi la Ngwea na kuangusha dua fupi.
Hata hivyo, baada ya yote hayo, kundi hilo la Wema na watu wake hatimaye walifanya dua fupi ya kumuombea malazi mema Albert Mangweha.
KUMBUKUMBU MUHIMU
Mangweha alikuwa msanii wa Bongo Fleva. Akiwa na miaka 31 alifariki dunia, Mei 28, 2013 nchini Afrika Kusini. Chanzo cha kifo chake inadaiwa ni matumizi yaliyopitiliza ya madawa ya kulevya. Alizikwa Morogoro, Tanzania, Juni 6, 2013.
0 comments:
Post a Comment